TAARIFA KWA UMMA-Minjingu Mines

Minjingu Mines and Fertiliser Ltd.

30/04/23

Descriptions



TAARIFA  KWA UMMA



Uongozi wa Kampuni ya 
uzalishaji, usambazaji na uuzaji 
wa mbolea Minjingu Mines and Fertiliser Limited (MMFL) unapenda kutoa
ufafanuzi wa tuhuma zilizoelekezwa kwenye Kampuni katika vyombo mbalimbali vya
habari ikiwemo mitandao ya kijamii. Tuhuma hizo zilihusu upatikanaji wa mifuko
776 ya mchanga kwenye ghala letu lilloko mjini Njombe. Maelezo yetu ni kama
haya yafuatayo:



Kwamba: kampuni ya MMFL ambayo ni kampuni ya
uzalishaji wa mbolea aina mbali mbali ni ya Kitanzania iliyojijengea heshima ya
uzalishaji na usambazaji wa mbolea ndani na nje ya nchi kwa kipindi cha miaka
22. Tunautaarifu umma kwamba hatujawahi kuhujumu wakulima au wadau wa kilimo
kwa kuzalisha na au kufungasha mchanga/udongo katika mifuko yake kama mbadala
wa mbolea. Aidha kampuni imeendelea kuwa na ushirikiano wa karibu na Serikali
katika kuhakikisha kwamba wakulima wanapata mbolea ya ruzuku kwa wakati na kwa
bei nafuu.



Kwamba: Afisa Mauzo wa MMFL kituo cha Njombe
-Bwana Gervas John Mtitu alipatikana na upotevu wa mbolea jambo ambalo
alilikiri. Baada ya upotevu huo, Bwana Gervas John Mtitu aliendelea kutoonyesha
ushirikiano licha ya jitihada mbali mbali za kumtafuta.



Kwamba: baada ya kutoendelea kupata
ushirikiano kutoka kwa Bwana Gervas John Mtitu, tarehe 28/1/2023, Kampuni
ilitoa  taarifa Kituo cha Polisi Njombe
mjini kuhusiana na upotevu wa mbolea  na
kutoonekana kazini ambapo tulipatiwa RB No. NJ/RB/390/2023.



Kwamba: tarehe 20/2/2023, Polisi walifika kwenye ghala  na kumweleza Afisa Masoko wa MMFL kwamba
walifika kufanya ukaguzi  baada ya kupata
taarifa kwamba kulikuwa na baadhi ya mifuko ambayo haikuwa na mbolea bali
bidhaa nyingine. Katika ukaguzi huo, walibaini kwamba kwenye ile mifuko ya
zamani (ambayo iliachwa na Bwana Gervas John Mtitu) , kulikuwa na mifuko yenye
mchanga. Afisa Masoko wa Kampuni alichukuliwa na Polisi na ghala kufungwa na
kuwa chini ya ulinzi wa Polisi.



Kwamba: tarehe 23/2/2023, maafisa wa TFRA
kutoka Kanda ya Mbeya walifika  na baada
ya hapo, maafisa wa TFRA, Polisi na maafisa kutoka MMFL walifika kwenye ghala
na baada ya uchunguzi, walibaini kuwepo na mifuko 776 ya mchanga ikiwa kwenye
mifuko ya zamani ya mbolea ya Minjingu. Ili mifuko hiyo ya mchanga kutoonekana
kiurahisi, mifuko ya mbolea halisi (ile ya zamani) ilizungushwa pande zote ili ionekane
kwamba yote ilikuwa mbolea.



Kwamba: TFRA 
waliiandikia MMFL barua  tarehe
24/2/2023 ambapo  maudhui ya barua
ilikuwa ni kukutwa na bidhaa ambayo siyo mbolea na Kampuni ilipigwa faini ya
shilingi milioni 30. Kampuni ililipa faini hiyo tarehe 25/2/2023.



Kwamba: MMFL imesikitishwa suala hilo (ambalo Mamlaka
inayohusika Kisheria ilishalitolea maamuzi) kuletwa tena tarehe 5 Machi 2023
kwenye jamii na kuleta sintofahamu kwa jamii.



Kwamba: katika jitihada za kuhakikisha
wakulima wanapata mbolea kulingana na uhitaji wa virutubisho wa zao, MMFL
imekuwa ikishirikiana na Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (TARI) na kutokana na
jitihada hizo, Kampuni imeweza kuzalisha mbolea maalum kwa ajili ya mazao ya
chai, kahawa, tumbaku, pamba na mazao ya chakula.Tutaendelea kufanya kazi kwa
karibu na Taasisi za Utafiti ili mazao mengi zaidi yaweze kuwa na mbolea
zinazokidhi mahitaji ili kuongeza tija.



Kwamba: kutokana na ubora wa mbolea zetu, Kampuni imekuwa
ikiuza mbolea zake Kenya, Burundi, Rwanda na Uganda na hakujawahi kuwa na
malalamiko yanayohusiana na ubora wa mbolea na mahitaji kwenye nchi hizo
yamekuwa yakiongezeka.



 



Hivyo:



·       
Tunawahakikishia
wakulima wote wa Tanzania kwamba Kampuni ya MMFL itaendelea kuwapatia wakulima
mbolea zenye ubora.



·       
Tuko
tayari kushirikiana na vyombo vya dola katika kuhakikisha kwamba mtuhumiwa
anapatikana na kupelekwa kwenye vyombo vya sheria.



·       
Kampuni
inaamini kwamba mhusika atakapopatikana, atasaidia kutoa taarifa ambazo
zitasaidia kujua kama haya yaliyojitokeza ni jitihada za yeye peke yake au kuna
hujuma ili kuidhoofisha kampuni ya MMFL.



Tunamhakikishia Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania –
DKt Suluhu Samia Hassan na Serikali yote kwamba Kampuni ya MMFL itaendelea
kuwahudumia wakulima wa Tanzania na wa nchi ambazo wanatumia bidhaa zetu kwa
kuwapatia mbolea zilizo na ubora.



 



Imetolewa na :-



Kurugenzi ya Mawasiliano



Minjingu Mines & Fertiliser LTD




Fanya Biashara yako ikue zaidi.

CATEGORIES

Apply For An Advert.


Email